TAMKO
LA CHAMA CHA WAANDISHI WA HABARI MKOA WA MBEYA (MBPC) DHIDI YA JESHI LA POLISI
NCHINI.
Chama cha waandishi wa Habari Mkoa
wa Mbeya (MBPC)kimepokea kwa masikitiko taarifa ya mauaji ya Mwandishi na
Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa habari Mkoa wa Iringa, Daudi
Mwangosi yanayodaiwa kufanywa na Jeshi la Polisi Mkoani Iringa tarehe
2/9/2012. Kutokana na mauaji hayo na kutoridhishwa na nguvu kubwa kupita kiasi
inayotumiwa na polisi dhidi ya raia, Waandishi wa habari Mkoa wa Mbeya
wanaungana na waandishi wa habari nchini kusitisha kutoa taarifa za jeshi la
polisi hadi hapo jeshi hilo litakapokubali kuchukua hatua kali za kinidhamu kwa
polisi waliohusika kufanya mauaji hayo akiwemo, Kamanda wa polisi Mkoa wa
Iringa aliyeongoza operesheni hiyo.
Tamko hilo pia limeeleza wazi kuwa
muda umefika kuwe na mkataba maalumu wa kazi kati ya waandishi wa habari
na jeshi la polisi na kwamba atakayekiuka hatua za kisheria dhidi ya majukumu ya
kila chombo zichukuliwe hatua kali za uwajibishaji.
Ili kujenga dhana ya uwazi na
uwajibikaji,Waandishi wa habari Mkoa wa Mbeya wanamtaka Waziri wa mambo ya
ndani, Mkuu wa jeshi la polisi nchini (IGP) na Kamanda wa mkoa wa Iringa
wajiuzulu nyadhifa zao kwa kuwa wameshindwa kusimamia vyema usalama wa raia na
mali zao.
Pia Tamko hilo limebainisha mfumo wa
uundwaji wa tume ya kuchunguza kifo hicho haupaswi kuongozwa na Jeshi la polisi
kwa kuwa ndio waliohusika na mauaji hayo na kwamba tume huru itakayoundwa ipewe
muda maalumu ili majibu yapatikane mapema na kwa haraka na hatua za
kisheria zichukuliwe kwa wahusika.
Waandishi wa habari Mkoa wa Mbeya,
wanaamini kuwa Serikali na jeshi la polisi litachukua hatua stahiki kwa
waliohusika na mauaji ya Mwandishi Daudi Mwangosi, na pia Polisi
watajitathmini upya katika utendaji wa shughuli zake hasa katika udhibiti wa
vurugu na uzuiaji wa maandamano.
………………………………..
Christopher Nyenyembe,
Mwenyekiti MBPC.
Nakala ;
1.Mkuu
wa Mkoa wa Mbeya na Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama.
2.Inspekta wa Jeshi la Polisi(IGP).
3.Vyombo vyote vya Habari
Taarifa kwa vyombo vya habari, Septemba 03, 2012
Sikika imepokea kwa masikitiko
makubwa taarifa za kifo cha mwandishi wa habari wa kituo cha Channel Ten mkoani
Iringa, Daudi Mwangosi. Kwa
mujibu wa vyombo vya habari, marehemu Mwangosi alikuwa kazini akitimiza wajibu
wake wa kutafuta habari. Tumestushwa zaidi baada ya kuona picha za mnato
zikionyesha jinsi ambavyo mtu anayedaiwa kuwa ni mwandishi huyo akishambuliwa
na idadi kubwa ya askari polisi na baadae kupoteza maisha.
Katika siku za karibuni,
tumeshuhudia ongezeko la matumizi ya nguvu kupita kiasi yanayofanywa na jeshi
la polisi, ambayo siyo tu yanasababisha uharibifu mkubwa wa mali za wananchi
bali pia baadhi yao kupoteza maisha. Mfano, mwezi uliopita, tuliarifiwa kuwa
kijana aliyeuawa mkoani Morogoro alikuwa akiuza magazeti na wala hakuhusika
katika vurugu kwa namna yoyote. Vivyo hivyo, marehemu Mwangosi alikuwa akitimiza
wajibu wake wa uandishi wa habari.
Uhai ni haki ya kikatiba ya kila
Mtanzania. Hivyo, ni jukumu la polisi kulinda maisha na uhai wa wananchi wote
bila kujali itikadi au kazi zao. Hakuna sheria inayohalalisha kujeruhi, kutesa
wala kuua mwananchi yeyote kwa sababu tu ati amekataa kutii amri ya polisi.
Sikika inasikitishwa zaidi na utamaduni unaozoeleka ndani ya jeshi la polisi
kwamba matukio ya kujeruhi, kutesa au vifo ni halali iwapo wanasiasa au
wananchi hawakutii amri.
Kwa mtazamo wetu, amri ya serikali
au polisi haitakiwi kuwa juu ya Katiba inayolinda haki ya kuishi. Hivyo,
kisingizio cha kukiuka amri ya polisi hakitakiwi kuwa sababu ya kujeruhi wala
kuua binadamu yeyote. Hata kama polisi watatoa maelezo kukanusha kuwa picha ya
mtu anayeteswa si mwandishi, je wanayo haki ya kumjeruhi, kumtesa au
kumdhalilisha mtanzania yeyote kama inavyoonekana kwenye picha hizo?
Tangu matukio haya ya kujeruhi,
kutesa na hata kuua wananchi yalipoanza, hakuna hatua za dhati zilizochukuliwa
na serikali wala jeshi la polisi. Vitendo hivi vinavyofanywa na polisi siyo tu
vinapunguza imani ya jeshi hilo kwa wananchi, bali pia vinakiuka wajibu wa
msingi wa jeshi hilo ambao ni kulinda usalama wa raia.
Ni matumaini yetu kwamba
waliohusika na kifo cha Daudi Mwangosi na watanzania wengine waliopoteza maisha
katika mazingira ya aina hii, watachukuliwa hatua stahiki. Pia, maaskari
wanaoonekana katika picha hizo wakimtesa na kumnyanyasa raia wafikishwe kwenye
vyombo vya sheria ili iwe funzo kwa wengine.
Tunatoa pole nyingi kwa familia
na ndugu wa marehemu Daudi Mwangosi pamoja na tasnia ya habari hapa nchini. Mungu
ailaze roho ya marehemu mahala pema peponi, Amen.
Bw. Irenei Kiria
Mkurugenzi Mtendaji, Sikika, S. L. P 12183 Dar es Salaam,
Simu: +255 222 666355/57, Nukushi: 2668015, Barua pepe: info@sikika.or.tz, Tovuti: www.sikika.or.tz
Mkurugenzi Mtendaji, Sikika, S. L. P 12183 Dar es Salaam,
Simu: +255 222 666355/57, Nukushi: 2668015, Barua pepe: info@sikika.or.tz, Tovuti: www.sikika.or.tz
TAMKO
LA CHAMA CHA WAANDISHI WA HABARI MKOA WA DODOMA (CPC)
CHAMA cha waandishi wa habari
mkoa wa Dodoma (CPC)wamelaani vurugu zilizotokea juzi mkoani Iringa na
kusababisha kifo cha mwandishi wa habari wa kituo cha utangazaji cha Chanel Ten
Daud Mwangosi. Kauli hiyo ilitolewa na Katibu wa chama hicho Habel Chidawali
alipokuwa akitoa tamko hilo mbele ya waandishi wa habari mkoani hapa.
Chidawali amesema kuwa kamwe chama hicho hakikubaliani na nguvu kubwa iliyotumiwa na jeshi la polisi kwa ajili ya kumwaga damu ya mwandishi huyo ambaye hakuwa na hatia na kamwe jeshi la polisi haliwezi kujitetea kwa kudai kifo cha mwandishi huyo ni bahati mbaya. Amesema kuwa jeshi la polisi limekuwa likionyesha wazi wazi kuwa linatumia nguvu,ubabe na matumizi mabovu ya silaha za moto ambayo hayajaweza kusaidia siku zote na badala yake kinachoachwa ni maumivu na vilio kwa wananchi.
Katibu huyo amesema kama jeshi la polisi linatuliza ghasia hakuna siku hata moja haijatokea wakamuua kiongozi yoyote wa siasa ambao nivinara wa mikutano mbalimbali. Kwa upande wao wananchi mbalimbali mkoani hapa wamekemea nguvu kubwa inayotumika na Polisi katika vurugu mbalimbali zinazotokea. Wamesema tabia ya jeshi la polisi kutumia nguvu na silaha za moto ambazo zinasababisha vifo vya watu wasiokuwa na hatia.
Catheline Muhinte, amesema kuwa tukio lililofanywa na jeshi la polisi la kumuua mwandishi wa habari linaonyesha dhairi kuwa kwa sasa jeshi hilo linafanya kazi kwa kukiuka maadili ya malengo yao. Amesema katika mwonekano wa picha ambazo zinaonekana katika vyombo mbalimbali vya habari inaonyesha dhairi kuwa polisi walihusika moja kwa moja na kifo cha mwandishi huyo.
TAMKO LA JUKWAA LA WAHARIRI TANZANIA KUHUSU KUUAWA KWA DAUDI MWANGOSI
TAARIFA YA JUKWAA
LA WAHARIRI (TEF) KWA VYOBO VYA HABARI
KUHUSU KUUAWA KWA
MWANDISHI DAUDI MWANGOSI
UTANGULIZI:
1. Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), limepokea
kwa masikitiko makubwa kifo cha mwandishi wa habari wa Kituo cha Televisheni
cha Channel Ten, mkoani Iringa, Daudi Mwangosi.
2. Mwangosi ambaye pia alikuwa Mwenyekiti wa
Chama cha Waandishi wa Habari mkoa wa Iringa (IPC), aliuawa akiwa kazini jana,
Septemba 2, 2012, wakati polisi walipokuwa wakiwadhibiti wafuasi wa Chama cha
Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
3. Tukio hili linaiingiza Tanzania katika
historia mbaya ya ukiukwaji na ukandamizwaji wa uhuru wa habari, kwani ni kwa
mara ya kwanza tunashuhudia mwandishi wa habari AKIUAWA WAKATI AKITEKELEZA
MAJUKUMU YAKE YA KIHABARI.
4. Taarifa za awali zinaonyesha kuwa Mwangosi
kabla ya kufikwa na mauti saa 9.30 alasiri katika kijiji cha Nyololo, Mufindi,
alizingirwa na kushambuliwa na polisi waliokuwa katika eneo la tukio. Na hata
alipopiga kelele za kuomba msaada, hakusikilizwa na matokeo yake aliuawa na
kitu kinachodhaniwa kuwa ni bomu.
5. Kwa kushirikiana na Baraza la Habari Tanzania,
TEF tumechukua hatua za haraka za kuunda timu ya uchunguzi wa suala hilo,
ambayo itakwenda mkoani Iringa mapema kadri itakavyowezekana, ili kubaini
ukweli wa tukio hilo. Lengo la uchunguzi huo ni kuweka kumbukumbu sahihi
(documentation) ya tukio hilo la aina yake katika historia ya nchi yetu.
6. Matokeo ya uchunguzi huo pamoja na mwingine
unaofanywa na Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC), ndiyo
yatakayotoa mwelekeo wa hatua ambazo TEF inachukua dhidi ya Jeshi la Polisi
katika siku chache zijazo.
MTIZAMO
NA MSIMAMO WA TEF
Kwa
kuzingatia taarifa kutoka Iringa na zile za vyombo vya habari vya jana
(Jumapili, Septemba 02, 2012) na leo (Jumatatu, Septemba 03, 2012), TEF ina
mtizamo na msimamo kama ifuatavyo:
1.
Kwanza tunalaani
vikali tukio la kupigwa, kisha kuuwawa kwa mwandishi Daudi Mwangosi ambalo
limeigusa tasnia ya habari kwamba sasa pengine waandishi wa habari ni malengo
“target ya polisi” wanapokuwa kwenye kazi zao.
2.
Ieleweke
wazi kwamba matukio haya siyo yanaondoa imani ya waandishi wa habari kwa jeshi
la polisi tu, bali yanaweza kuwa chanzo cha uhasama na ufa mkubwa ambao utawanyima
wananchi nafasi ya kutumikiwa na pande mbili ambazo zinategemeana.
3.
Kwa matukio ya
aina hii, tunadhani wakati mwafaka kwa uongozi wa Jeshi la Polisi nchini
kuwajibika, kuazia kwa Kamanda wa Polisi wa Mkoa na uongozi wa Makao Mkuu, akiwamo
Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Saidi Mwema.
4.
Tunasema hivi
kwani kuna kila dalili kwamba polisi wanahusika kwa namna moja au nyingine na
tukio au/na matukio yaliyosababisha kifo cha Mwangosi, kwani kitendo cha
kumzingira tu na kumshambulia kinathibitisha kwamba hawakuwa na nia njema hata
kidogo dhidi ya mwandishi huyu.
5.
Taarifa ambazo
TEF tunazo, pia zinadai kwamba kulikuwa na mpango wa polisi wa
“kuwashughulikia waandishi wa habari watatu” (Mwangosi) akiwa mmojawapo na hilo
lilionekana likitekelezwa kwa polisi kumshambulia mwandishi huyo, baadaye
alipoteza maisha katika mazingira ya kutatanisha.
6.
Hili linatiliwa
nguvu na tukio jingine la polisi kumpiga na kumjeruhi mwandishi mwingine,
Godfrey Mushi ambaye ni mwakilishi wa gazeti la Nipashe mkoani Iringa.
Mwandishi wa tatu ambaye hadi tunapoandika taarifa hiyo yumo katika mpango wa
‘kushughulikiwa na polisi’ ni Francis Godwin ambaye ni mwandishi wa habari wa
kujitegemea.
7.
Vitendo vya aina
hii havivumiliki na havipaswi kuachwa kuendelea kwani ni hatari kwa ustawi wa
demokrasia na uhuru wa habari nchini. Hatuwezi kuendelea katika mazingira
ambayo polisi wanageuka kuwa chombo cha mauaji ya raia badala ya kuwa walinzi
wa raia.
8.
Kwa maana hiyo,
mbali na uchunguzi ambao utafanywa na polisi, tunatoa wito kwa Serikali kuunda
chombo huru, ambacho kitabaini ukweli, na matokeo yake yatangazwe kwa umma,
huku wahusika wa aibu hiyo wakichukuliwa hatua za kisheria. Tunasema hivyo,
tukifahamu kwamba tayari kuna jitihada za kuficha ukweli na kueneza propaganda
za uongo kuhusu tukio zima.
9.
Mwenendo wa aina
hii wa chombo cha dola kuamua kutumia silaha kuua na baadaye kupanga mbinu
chafu za kuficha ukweli ni hatari kwa Taifa, na unaiweka demokraisia ya nchi
yetu njia panda, huku tukielekea katika hatari ya Taifa kutumbukia katika uovu.
IMETOLEWA NA:
NEVILLE MEENA,
KATIBU MKUU –
JUKWAA LA WAHARIRI TANZANIA (TEF)
SEPTEMBA 3, 2012
KIFO CHA MWANDISHI TANZANIA: POLISI
WATAKIWA KUWAJIBIKA
Waandishi
wataka uongozi wa jeshi la polisi Tanzania kuwajibika kuanzia kamanda wa polisi
wa mkoa na uongozi wa makao makuu akiwamo -IGP, Saidi Mwema. Viongozi wa vyama
vya siasa, wanaharakati, waandishi wa habari na wananchi wa kawaida jijini Dar
es salaam, wamezungumzia tukio la kuuwawa kwa mwandishi mmoja
wa habari Daudi Mwangosi katika vurugu zilizotokea jumapili mkoani Iringa zilizohusisha
jeshi la polisi na wafuasi wa chama cha upinzani cha CHADEMA. Watu wengi
waliohojiwa kuhusu kifo cha mwandishi huyo walidai kuwa mauaji hayo yametokana
na polisi kutumia nguvu kupita kiasi, huku wakitaka tume huru iundwe ili
kufanya uchunguzi wa kina wa chanzo kilichopelekea kifo cha mwandishi huyo.
Wakati huo huo jukwaa la wahariri kwa kushirikiana na Baraza la Habari Tanzania, wameunda timu ya uchunguzi wa suala hilo ambayo itakwenda mkoani Iringa ili kubaini ukweli wa tukio hilo. Lengo la uchunguzi huo ni kuweka kumbukumbu sahihi ya tukio hilo. Katika tamko lake Jumatatu, jukwaa hilo la wahariri limesema tukio la mauaji ya mwandishi wa habari linaiingiza Tanzania katika historia mbaya ya ukiukwaji na ukandamizwaji wa uhuru wa habari, kwani ni kwa mara ya kwanza nchi inashuhudia mwandishi wa habari akiuwawa wakati akitekeleza majukumu ya kazi yake Naye kaimu katibu mkuu wa chama cha UDP, Isaac Cheyo ametaka jeshi la polisi kuacha kutumia nguvu kupita kiasi wakati wa kutuliza ghasia. Amawataka polisi kuacha kutumika jeshi hilo kama chombo cha kuweka mbele maslahi ya watawala badala ya umma wa watanzania.
Pia mwenyekiti wa chama cha siasa cha NLD Dk.Emmanuel Makaidi, ametaka kuwepo kwa chombo huru cha kuchunguza matukio yanayohusisha jeshi la polisi kuliko ilivyo hivi sasa, jeshi kuunda timu ya uchunguzi kujichunguza yenyewe. Daudi Mwangosi licha ya kuwa mwakilishi wa kituo cha televisheni cha channel Ten cha jijini Dar es salaam alikuwa mwenyekiti wa klabu ya waandishi wa habari mkoani Iringa. Waandishi wametaka uongozi wa jeshi la polisi nchini Tanzania kuwajibika kuanzia kamanda wa polisi wa mkoa na uongozi wa makao makuu, akiwamo Mkuu wa Jeshi la Polisi -IGP, Saidi Mwema. Mwandishi huyo wa habari anatarajiwa kuzikwa jumanne Tukuyu Mkoani Mbeya.
Wakati huo huo jukwaa la wahariri kwa kushirikiana na Baraza la Habari Tanzania, wameunda timu ya uchunguzi wa suala hilo ambayo itakwenda mkoani Iringa ili kubaini ukweli wa tukio hilo. Lengo la uchunguzi huo ni kuweka kumbukumbu sahihi ya tukio hilo. Katika tamko lake Jumatatu, jukwaa hilo la wahariri limesema tukio la mauaji ya mwandishi wa habari linaiingiza Tanzania katika historia mbaya ya ukiukwaji na ukandamizwaji wa uhuru wa habari, kwani ni kwa mara ya kwanza nchi inashuhudia mwandishi wa habari akiuwawa wakati akitekeleza majukumu ya kazi yake Naye kaimu katibu mkuu wa chama cha UDP, Isaac Cheyo ametaka jeshi la polisi kuacha kutumia nguvu kupita kiasi wakati wa kutuliza ghasia. Amawataka polisi kuacha kutumika jeshi hilo kama chombo cha kuweka mbele maslahi ya watawala badala ya umma wa watanzania.
Pia mwenyekiti wa chama cha siasa cha NLD Dk.Emmanuel Makaidi, ametaka kuwepo kwa chombo huru cha kuchunguza matukio yanayohusisha jeshi la polisi kuliko ilivyo hivi sasa, jeshi kuunda timu ya uchunguzi kujichunguza yenyewe. Daudi Mwangosi licha ya kuwa mwakilishi wa kituo cha televisheni cha channel Ten cha jijini Dar es salaam alikuwa mwenyekiti wa klabu ya waandishi wa habari mkoani Iringa. Waandishi wametaka uongozi wa jeshi la polisi nchini Tanzania kuwajibika kuanzia kamanda wa polisi wa mkoa na uongozi wa makao makuu, akiwamo Mkuu wa Jeshi la Polisi -IGP, Saidi Mwema. Mwandishi huyo wa habari anatarajiwa kuzikwa jumanne Tukuyu Mkoani Mbeya.
No comments:
Post a Comment