BM BARBERSHOP KINONDONI

Tuesday, September 4, 2012

UHABA WA MADAKTARI NA WALIMU WILAYA YA MUHEZA NI ISSUE

na Bertha Mwambela, Muheza
HALMASHAURI ya Wilaya ya Muheza mkoani Tanga inakabiliwa na ukosefu wa walimu na madaktari, na kwamba hali hiyo imesababisha kudorora kwa sekta ya elimu na afya.Kauli hiyo ilitolewa jana na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Muheza, Amir Kiroboto wakati wa kikao cha kwanza cha Baraza la Madiwani kwa mwaka wa fedha 2011/2012.
 
Alisema ukosefu huo wa rasilimali watu katika idara hizo mbili nyeti ni wa muda mrefu kwa zaidi ya miaka minne mfululizo, hivyo kuwafanya washindwe kufikia malengo katika utendaji wao wa kazi.“Inanisikitisha kuona kuwa ni zaidi ya miaka minne mfululizo tumekuwa na tatizo hili, shule tunazo, zahanati pia tunazo, lakini hazina madaktari. Kwa kweli inaumiza sana, hivyo inabidi kwa umoja wetu tusaidiane katika kupunguza au kumaliza kabisa tatizo hili,” alisema Kiroboto.Aliwapongeza madiwani na watendaji wa halmashauri hiyo kwa kusimamia vizuri majukumu yao na hivyo kusababisha halmashauri hiyo kupata hati safi mara tatu mfululizo.
 
Alisema anaamini kuwa mshikamano, upendo na umoja ndiyo nguzo pekee iliyoweza kuwafikisha hapo walipo kwa sasa kwa kuwa Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) amekuwa akifanya kazi bila ya kukutana na tatizo lolote katika halmashauri hiyo.Nae Mkuu wa Wilaya hiyo, Subira Mgalu aliwataka madiwani kutimiza vema wajibu wao wa kuwatumikia wananchi katika maeneo yao ya kazi, kwani kwa kufanya hivyo kutasaidia kuwanyima nafasi wapinzani katika kuikosoa serikali, ambao alisema kwa sasa anawafananisha na walimu katika kufuatilia mambo yanayohusu jamii kwa ukaribu.
 
“Naamini kuwa siasa za sasa zimebadilika hivyo madiwani tuwe makini katika utendaji ili tuwanyime nafasi wapinzani wetu ambao wao muda wote wamekuwa makini kutufuatilia na kuikosoa serikali iliyoko madarakani,” alisema Mgalu.

Chanzo: Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment