BM BARBERSHOP KINONDONI

Monday, October 29, 2012

MWANATANGA ASHIRIKI KWENYE UZINDUZI WA TRENI KAMA MDAU WA USAFIRI LEO JIJINI DAR ES SALAAM




USAFIRI wa treni jijini Dar es Salaam kutoka Ubungo Maziwa kuelekea katikati ya Jiji la Dar es Salaam (Stesheni ya Treni) umeanza leo rasmi baada ya kuzinduliwa na Waziri wa Uchukuzi Mheshimiwa Dr. Harrison Mwakyembe. Treni ya kwanza imeondoka Ubungo majira ya saa 12:00 asubuhi kuelekea katikati ya jiji, ambapo kwa mujibu wa maofisa wa Shirika la Reli Tanzania (TRC) treni hiyo imetumia wastani wa dakika 30 kufika katikati ya jiji.

Treni iliyoanza kazi leo ina injini mbili (vichwa vya treni) moja ikiwa imefungwa nyuma na nyingine mbele huku ikiwa na mabehewa sita, yaani matano ya abiria wa kawaida (watu wazima) na moja likiwa ni maalumu kwa ajili ya kubeba wanafunzi.  Nauli kwa kila abiria mmoja ni sh. 400 kwa tripu huku wanafunzi wakitakiwa kulipa sh. 100.

Waziri wa Uchukuzi, Mheshimiwa Dk Harrison Mwakyembe amezindua usafiri huo leo kama majaribio akiwa pamoja na viongozi waandamizi kutoka TRC, Mamlaka ya Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA), TAZARA pamoja na Polisi Kitengo cha Reli. Treni hiyo imezinduliwa sambamba na treni ya TAZARA ambayo itafanya kazi kama ya Ubungo, lakini yenyewe ikianzia eneo la TAZARA kuelekea Mwakanga.

Akizungumza mara baada ya uzinduzi huo Waziri Mwakyembe alisema atahakikisha treni hiyo inaendelea kufanya kazi ili kuwasaidia kiusafiri wananchi wa Dar es Salaam ambao wamekuwa wakisumbuliwa na kero ya usafiri hasa kwa foleni, ambapo hutumia muda mrefu njiani wakati wa kuingia na kutoka jijini. Dr. Mwakyembe alisema jumla ya mabehewa 14 pamoja na injini mbili zimekarabatiwa na mafundi wazalendo nchini, ambayo ndiyo yatakayokuwa yakifanya kazi ya kusafirisha abiria kuingia na kutoka jijini kila asubuhi na jioni. Kwa sasa treni moja imeanza kwa majaribio lakini baada ya uzinduzi mkubwa treni mbili zitafanya kazi, na zitakuwa zikipishana njiani moja ikirudi na nyingine ikienda.

Akifafanua zaidi alisema kitendo cha mafundi wazalendo kufanya ukarabati kwa mabehewa na injini kimeokoa kiasi kikubwa cha fedha za umma kwani ukarabati wote umetumia sh. bilioni 2.1 tu, wakati kama Serikali ingelazimika kukodi injini gharama ingekuwa kubwa zaidi kwani bei ya kukodi injini moja ya treni ni sh. milioni moja kwa siku. Hata hivyo Waziri Mwakyembe amewataka Watanzania hasa abiria kuwa wavumilivu kwa upungufu utakaojitokeza kwa safari za mwanzo kwani bado wanaendelea kufanya marekebisho kadhaa, lakini baada ya muda mambo yatakaa sawa. Mwanatanga alikuwa mmoja wa wasafiri walioizindua treni hiyo leo.

Mmoja wa viongozi waandamizi wa TRC, alisema treni hiyo itafanya kazi kila siku isipokuwa kwa siku za jumapili na siku kuu na itakuwa ikianza safari zake saa 12:00 asubuhi hadi saa sita mchana na kupumzika hadi saa 9:00 jioni, itakapoendelea tena na safari zake hadi majira ya saa nne usiku. Behewa moja la treni linauwezo wa kuchukua abiria 66 wakiwa wamekaa likiwa na milango minne, feni, taa, muziki/redio, pamoja na mikanda maalumu ya kujishikia kwa abiria ambao watakuwa wamesimama.

Aidha mabehewa yote yana madirisha ya kutosha kuingiza na kutoa hewa ya kutosha. Treni ilioanza kazi leo, ikitokea Ubungo ilikuwa ikisimama vituo vya eneo la Mwananchi (relini), Tabata Relini, Buguruni Miamani, Tazara, Kariakoo Gerezani (Kamata), na mwisho Kituo Kikuu cha Treni kilichopo jirani na Kituo cha Polisi Kati (Katikati ya Jiji).









No comments:

Post a Comment